HATIMA YA KIMUNGU SEHEMU YA 26.

Image
  HATIMA YA KIMUNGU SEHEMU YA 26. Ilipoishia.......... Alipomgeuza tu alishangaa kuona sura ya yule binti ni ya mbuzi. Aliogopa na kudondoka chini kwa kelele kuu alilia 'maaamaaaaaaa!!!!" Alijiokotaokota huku akiangukaanguka mpaka kwenye gari yake. Alipanda ndani ya gari na kuwasha gari. Alikimbiza gari mpaka akafika karibu na geti la nyumba ya Elvine, lakini kabla hajafika getini alishangaa kuona anaguswa mabegani ndani ya gari lake. Alitoa macho kwa uoga na mshtuko mkubwa mpaka akakosea njia na kwenda kugonga mti... Kusoma sehemu ya 25 bonyeza hapa. Sasa inaendelea......, Aligonga mti kwa nguvu mpaka naye akajipigiza kichwa kwenye usukani wa gari na gari ikaharibika sana upande wa mbele, alipona kwa neema tu kwa namna gari ilivyokuwa mwendo kasi angeweza hata kupoteza maisha lakini haikuwa hivyo. Alijikaza na kushuka kwenye gari akakimbia kuelekea kwenye nyumba ya Elvine,  njiani alikumbwa na kimbunga cha ajabu sana. Baada ya kile kimbunga kumpitia na kumzingazinga kwa muda

SIMULIZI YA KUSISIMUA KUHUSU “HATIMA YA KIMUNGU”. >>SEHEMU YA TATU.

 

SIMULIZI YA KUSISIMUA KUHUSU “HATIMA YA KIMUNGU”.

>>SEHEMU YA TATU.

 Ilipoishia....,..

Editrin baada ya kutulia alimsimulia kisa kizima mama yake tangu alipotoroka kwao, hadi kufikia hapa alipo na namna ambavyo Elvine alivyopotea. Eliana alionesha kuumia sana kwani kwa namna nyingine tunaweza kusema yeye ndiye aliyekuwabibi wa mtoto yule. Wakiwa wanaendelea na mazungumzo yale Editrin akaanza kukumbuka kisa chote kilichomkuta kwenye maisha yake hata kupelekea yeye kutoroka kwao Dar es salaam na kuamua kuja kuishi Iringa.......

 Kama hujasoma sehemu ya kwanza na ya pili bonyeza hapa.

Sasa inaendelea...,....

Editrin alizaliwa Katika familia ya kitajiri sana. Baba yake alikuwa akiitwa Mr. Edward na mama yake aliitwa Eliana. Katika familia yao walizaliwa watoto wawili tu! ambao ni Editrin na Edger. Tangu utoto wao walipendwa sana na wazazi wao wote wawili. Editrin na kaka yake Edger hawakuwahi kuyajua maisha ya shida maana baba yako alikuwa na pesa sana. Walikuwa wakiishi jijini Dar es salaam ambako baba yao alikuwa ni mmiliki wa mabasi ya "A quality bus".

      Kampuni ya Mr. Edward ilipendwa sana na watu wengi, maana ilisifika kwa kuwa na wahudumu wakarimu na safari za uhakika.

     Editrin baada ya kumaliza sekondari katika shule ya st. Claudy, alichaguliwa kujiunga na kidato shule ya serikali iliyoitwa "Kugilwa high school" iliyopo jijini Dodoma. Akiwa shule alikutana na kijana mmoja alieitwa(aliyeitwa) Edwin ambaye alikuwa ni kijana wa kipentekoste na alikuwa ni mtu wa imani sana. Kijana yule alikuwa ni mcheshi sana na alipendwa na kila mtu, alipenda utani lakini pia, alipenda kuwashuhudia watu wa kila namna na hakusita kuwaambia hata walimu habari za Yesu kwa namna alivyokuwa anajiamini. Kila mtu alimpenda. Kwani, hakuwa msema uongo wala hakupenda ugomvi.

     Kwa upande wa Editrin katika familia yao walikua ni waroma tena wale ambao ibada kwao sio lazima labda kuwe na tukio maalumu kanisani ndipo watakwenda na sio ajabu kabisa bado watatoka ibada ikiwa haijakwisha. Hata baada ya kufika shule bado hakuwa  anapenda ibada japo ibada zilikuwa zikifanyika kila siku, lakini alikuwa radhi akajifiche chooni hadi muda wa ibada uishe kisha aende darasani kusoma yaani prepo.

     Mkuu wa shule yao alikuwa ni mwanamke aliyeitwa Emmy . Emmy alikuwa mtu wa dini sana na ndiye aliyekuwa mlezi wa Casfeta pale shuleni, hivyo mama huyo aliweka sheria kuwa hakuna mtu kuwepo bwenini muda wa vipindi vya dini, kila mtu anatakiwa kuwepo kwenye dini yake ifikapo saa 1:00 hadi saa 2:00 usiku.

     Sheria za Emmy zilimkera sana Editrin hivyo alimwambia baba yake kuwa anahitaji kuhama shule ile. Wakati akiwa katika mipango hiyo mwalimu wao wa darasa aliyeitwa Emily alibadilisha ukaaji wa watu katika darasa lake hivyo Editrin akajikuta anakaa na Edwin sehemu moja.

     Kwa ucheshi wa Edwin alimzoea kwa haraka sana Editrin na wakawa marafika sana. Edwin aligundua kuwa Editrin alikuwa ni binti asiyependa ibada hata kidogo, alianza kumshawishi hata kwa zawadi; alimuahidi kuwa akienda kuwatembelea Casfeta kwa muda wa wiki moja basi atampa zawadi nzuri sana.

      Kwa ule ushawishi wa Edwin, Editrin alivutiwa kwenda kusali ili apewe tu ile zawadi. Alipokwenda mara ya kwanza tu, alijikuta anaifurahia ibada ya Wanacasfeta wa pale shuleni, maana ilikuwa ni siku ya vishirikishi na kusifu. Alishangaa kuona kuwa Edwin alikuwa ni mwimbaji mzuri sana na ndiye aliyekuwa mwenyekiti wa Casfeta tawini hapo.

     Alizidi kwenda kila siku, na aliweza aligundua kitu kingine kuwa licha ya Edwin kujua kuimba pia alikuwa muhubiri na mshauri mzuri sana kwa watu wengine pale shuleni.

   Siku moja katika ibada ya jumapili usiku ambayo ndiyo ilikuwa siku ya mwisho ili apate zawadi yake, Edwin alitoa somo ambalo lilimgusa sana Editrin. Somo hilo lilikuwa linahusu kuweka misingi imara kwa watoto na familia. Na katika maelezo alisema "kuna watu leo hawampendi Mungu kwa sababu ya misingi waliyojengewa toka wakiwa wadogo na familia zao". Maneno yale yalimgusa sana Editrin na alihisi kama yeye ndiye anayeambiwa maneno yale. Alilia sana na kwa siku chache zile alizoshiriki ibada alijiona kama mkosaji sana kwani alijifunza vitu vingi sana hasa kuhusu Mungu. Editrin aliamua kuokoka na kubadili maisha yake ya mwanzo. Edwin alifurahi sana kuona kaweza kumfanya rafiki yake aokoke na yeye mwenyewe Edwin ndiye alimuongoza sara ya toba na kumwombea Editrin.

     Tangu siku hiyo Editrin na Edwin wakawa marafiki wakubwa sana. Edwin kwakuwa alimuahidi rafiki yake zawadi alikwenda kumnunulia saa ya 5000/= na ulipofika muda wa prepo baada ya kutoka kwenye kipindi cha dini, Edwin alimpatia ile saa Editrin.

    "Saa? Mbona inaonekana ya bei ndogo sana hii!!. Asee!! mimi siwezi kuvaa hii, labda unipe zawadi nyingine" Editrin alijibu kwa dharau kidogo kuonesha hakuridhika na zawadi aliyopewa. Edwin hakujibu chochote bali aliichukua ile saa na akairudisha mfukoni mwake kisha akalala kwenye dawati mpaka prepo ilipoisha na ilipogongwa kengere tu aliondoka bila hata kuaga.

     Ukweli ni kuwa Edwin hakuwa mtoto aliyetoka katika familia ya kitajiri kama Editrin. Yeye kwao kulikuwa ni palepale Dodoma wilaya ya Mpwapwa na kwao walikuwa ni masikini kabisa. Na zawadi ile ilimgharimu sana maana ilimpasa atoe pesa yake yote ya matumizi aliyokuwa katumiwa na baba yake mlezi kwani aliona hakuna shida kama atatoa kwaajili ya rafiki yake huyo maana chakula shuleni walipewa bure. Aliamua kufanya hivyo kwakuzani kuwa atamfurahisha sana rafiki yake na pia atamtia moyo kwa uamuzi wake wa kuokoka na kuanza kusali. Lakini daah!! haikuwa kama alivyotarajia maana, Editrin alizoea kupewa zawadi za gharama sana kwao, kwahiyo ile zawadi kwake haikumpendeza kabisa. Ni kweli editrin aliokoka lakini bado kuna vitu alikuwa hajui kama ni kosa hivyo alihitaji kujifunza zaidi maana kuna mambo bado alikuwanayo.

     Toka siku hiyo Edwin alikuwa mpole sana. Alijiona yeye ni wachini sana kwakuwa kwao hawana pesa. Alijishusha thamani na furaha yote ilipotea, akawa ni mtu wakujitenga muda wote.

    Hali ile ilimshangaza kila mmoja maana ilikuwa ni ghafla sana kutokea. Editrin pia alishangazwa na badiliko lile na hata alipomuongelesha Edwin alijibu kwa kifupi sana, na hakupenda kupiga naye stori kama ilivyokuwa mwanzo.

     Editrin alishangaa kwani hakuwa anajua kuwa yeye ndiye wamwisho kumfanya Edwin akose amani na kubadilika vile maana kwake aliona ilikuwa kawaida tu.

    Edwin akawa anajitenga sana na hata muda wa ibada alikuwa anakaa nyuma na hata katika maombi alionekana kuomba kwa uchungu sana. Licha ya kuwa mwenyekiti lakini, alikuwa hapendi sana hata kusimama mbele ya watu tena kama mwanzo, hili liliwaumiza wengi na walipomuuliza hakujibu chochote.

     Baada ya wiki mbili kupita Editrin alipewa taarifa kuwa uamisho umekamilika hivyo siku inayofuata ambayo ni siku ya jumatatu anatakiwa kuondoka  shuleni hapo. Ile taarifa ilimuumiza sana Editrin maana alijikuta hatamani tena kuondoka. Ilipofika usiku wakiwa prepo Editrin alisimama mbele ya darasa na kuaga darasa kwa kusema kuwa jumatatu ambayo ndiyo siku inayofuata alikuwa anaondoka kuelekea Dar es salaam ambako ndiko atakuwa anasoma.

      Edwin alishangaa sana maana hakuwa anajua. Editrin alipomaliza kuaga alirudi kukaa kwenye siti yake karibu na Edwin.

     "Hivi ni kweli unaondoka?" Alihoji Edwin akiwa haamini.

     "Ndiyo"

     "Kwanini?"

     "Nilishamwambia baba kuwa nataka kuondoka kwahiyo uhamisho umekamilika. Japo ni muda kidogo kwahiyo hata mimi nilikwisha sahau".

     "Kwanini uondoke?"

     "Aa... Hapa sikupapenda tu, japo kwasasa nilitamani kubaki ila sina jinsi tena"

     "Anhaa. kwani baba yako anafanya kazi gani?" Edwin alihoji huku anatazana taftari lake bila kujua kwanini kauliza.

     "Ni mmiliki wa mabasi ya 'A quality"

     "Anhaaa ndiyo maana"

     "Ndiyo maana nini?"

     "Hivi mimi na wewe si tunakaa dawati moja, ulishindwa kuniaga mimi kwanza?"

     "Sasa unadhani ningekwambiaje mtu hutaki kuongea na mimi?"

     "Editrin wewe unadharau sana, kweli nakwambia. Na usipo jirekebisha hutofika sehemu salama". Aya basi sawa nenda. Na uwasalimie ukifika" Edwin aliongea vile kwa upole sana na alionesha kuwa anaelewa vyema anachosema.

     "Halafu mbona kama unanichukia Edwin nilikufanyia nini wewe?" Aditrin aliuliza akiwa kaumia sana kuitwa mwenye dharau halafu na rafiki yake.

     "Hamna kitu. Am sorry, safari njema Mungu akutangulie". Edwin alisema hivyo na kuonyesha tabasamu la kujilazimisha kisha akatoka nje na hakurudi tena.

   Siku iliyofuata Editrin aliondoka na hakuweza kumuona rafiki yake toka usiku ule. Kile kitu kilimuumiza sana maana Edwin ndiye aliyekuwa mtu wa karibu sana na kibaya zaidi hata namba ya simu ya Edwin hakuweza kuipata, maana Edwin alishawahi kusema kuwa hana simu lakini Editrin alijua ni utani tu.

     Alipofika katika shule mpya alianza kujitahidi kuwa mtu wa ibada na hakuwahi msahau rafiki yake Edwin, licha ya kuwa waliagana vibaya sana. Editrin alijiona kuwa anabadilika tabia na kuwa mpole, mstaarabu, mwenye heshima, akawa na imani, lakini pia, akajua kusamehe. Mwisho akawa anajisemea mwenyewe, "mbona nakuwa na tabia nzuri kama Edwin?, Kwakweli Asante Mungu umenitoa mbali".

     Siku moja alimpigia mwalimu wao wa darasa wa "Kugilwa high school" na kumweleza kuwa alihitaji kuongea na Edwin. Mwalimu alimwambia kuwa kwawakati huo Edwin yupo kwenye mtihani ila akitoka atamwambia kuwa Editrin alihitaji kuongea nae.

     Ilipofika jioni mwalimu alimwita Edwin na kumweleza kuwa Editrin alihitaji kuongea nae. Lakini Edwin alikataa kwa kusema anaharaka labda wakati mwingine. Mwalimu alimtafuta Editrin na akamwambia kile Edwin alichojibu. Wakiwa wanaendelea kuzungumza madam Emily alijikuta anawiwa kumweleza Editrin kuhusu maisha ya Edwin. Alimwambia kuwa Edwin ni yatima anaishi na walezi tu ambao ndiyo kama wazazi wake lakini ukweli ni kuwa walikuwa ni ndugu wa baba yake. Na kifo cha wazazi wake kilitokana na umaskini maana baba yake alikufa kwa maleria tu lakini kwakuwa alikosa dawa alipoteza maisha, na mama yake pia hakuchukua muda akafa. Kwaiyo ni mtoto anayesomeshwa kwa msaada wa shirika la kiserikali. Madam Emily alimwambia vile Editrin ili kama angeweza basi amsaidie rafiki yake Edwin kwa chochote.

    Baada ya mazungumzo yale Editrin aliumia sana kwasababu  hakujua hilo kabla na ndipo akajua kwanini Edwin alikosa amani baada ya yeye kuidharau zawadi aliyopewa. hivyo aliazimia kumsaidia Edwin kwa siri.

    Aliongea na mwalimu na akamwambia kuwa atakuwa anamtumia hela Edwin laki 2 kila mwezi kupitia simu ya mwalimu lakini Edwin asijue. Mwalimu alifurahi sana kuona kuwa Editrin ana moyo wa kusaidia wengine kiasi kile.

      Editrin kweli akawa anatuma hela kila mwezi maana, kwao hela ilikuwa sio tatizo kwasababu kila mtoto aliwekewa pesa ya kutosha kwenye akaunti ya benk kila mwisho wa mwezi. Edwin akawa anashangaa hela zile zilitoka wapi, lakini mwalimu aliishia kusema mfadhiri wako katuma hela na hakuwahi kumwambia ukweli mpaka alipomaliza kidato cha sita.

     Editrin na Edwin walikuja kukutana tena chuo kikuu cha "Mzumbe-Mbeya" ambapo wote walikuwa wakisomea sheria na wakati huu Editrin alikuwa mtumishi mzuri sana sio kama mwanzo. Siku walipokutana ilikuwa kama ndoto kwa kila mmoja wao maana walikutana ibadani wakiwa wanajitambulisha muda wa ibada.

     Tokea hapo urafiki wao uliendelea na Editrin aliweza kuomba msamaha kwa rafiki yake Edwin. Kila mtu aliamua kusahau yaliyopita. Na wakati huu Edwin alikuwa kaanzisha mradi wa kufuga kuku wa kisasa kijijini kwao hivyo hakuwa anategemea misaada tena kwa mtu yeyote.

     Walijikuta wakipendana sana na wakaazimia kuoana pindi wakimaliza masomo.

     Baada ya kumaliza mwaka watatu Editrin alirudi Dar es salaam na akamwambia mama yake Eliana  kuhusu kuolewa na Edwin. Mama yake hakuwa na shida kabisa lakini ilikuwa tofauti sana kwa baba yake Mr. Edward ambaye alichukia sana baada ya kusikia taarifa zile  na alifoka sana.

     Baadaye Editrin aliambiwa  kumbe baba yake alikwisha muandaa mtu wa kumuoa binti yake. Kijana aliyechaguliwa alikuwa ni mtoto wa familia ya kitajiri iliyokuwa na urafiki na familia yao. Kijana huyo aliitwa Esau.

     Editrin hakuwahi kumpenda hata kidogo kijana huyo hivyo alimweleza mama yake na kaka yake kuwa hawezi kukubali kuolewa na Esau ambaye alikuwa ni kijana kutoka familia ya watu wenye pesa sana. Mr. Edward hakuwahi kumfokea binti yake wala kumlazimisha jambo, hata baada ya kusikia kuwa binti yake kawa mtu wa dini hakumzuia kabisa kusali bali alimpongeza tu na akawa anamtania sana kwa kusema Editrin saizi ndiyo kamjua Yesu kwahiyo anawazidi imani wote mule ndani. Lakini wakati huu, kila mtu alimshangaa maana alilazimisha kwa nguvu zote ndoa ifungwe.

Mr. Edward aliamua kuandaa harusi ya binti yake kwa lazima jambo ambalo hata Edger kaka wa Editrin hakulipenda.

Zikiwa zimebaki siku chache harusi kufungwa Edger aliomba namba ya Edwin kwa Editrin, maana Edger alikuwa anajua kuwa mdogo wake hampendi Esau na istoshe hata yeye hakuwa anampenda Esau kabisa. Hii ni kwasababu Edger alikuwa ni rafiki wa Esau na alizijua tabia za rafiki yake. Hivyo, bila kuwa na wasiwasi alikwishajua namna dada yake atakavyoteseka.

Editrin hakujua kwanini kaka yake kaomba namba ya Edwin. Wakati huo Edwin alikwisha pewa taarifa kuwa Editrin anaolewa na mtu mwingine na alikuwa amekata tamaa kabisa.

Siku moja Edwin alipigiwa simu na Edger na kuulizwa kuwa anapatikana wapi. Hakujua kwanini Edger anamtafuta lakini, kwakuwa Edger alijitambulisha vizuri kwake kuwa ni kaka yake Editrin, hakuona tatizo kumuelekeza. Edger alikwenda na gari lake hadi Dodoma-Mpwapwa na alipokelewa na Edwin stendi.

Baada ya kukutana tu Edwin aliingia kwenye gari la Edger na mlango ukafungwa. Wakiwa ndani ya gari Edger alimuuliza Edwin "unampenda Editrin kweli?" Swali lile lilimtoa machozi Edwin ambaye alionesha kukata tamaa lakini alijibu "ndiyo".

Baada ya kujibu tu, Edger aliwasha gari na kuanza kuondoka. Wakati Edwin anawaza kumuelekeza kwao, Alishangaa gari inawashwa kuelekea lami. Edwin alishituka sana maana hakujua wapi wanaelekea. Alipouliza, Edger alimjibu acha uoga kuna jambo la muhimu tunatakiwa kufanya leo kabla siku haijaisha. Edwin hakuwa amejiandaa kwa safari lakini akaona hana namna ya kukataa.

Walifika hadi Dar es salaam siku hiyo hiyo na ilikuwa ni usiku sana, muda kama wa saa 7:30 hivi za usiku.

Edwin hakuwai kufika Dar es salaam kwahiyo alikuwa akishangaa sana na hakujua wako wapi wala wanaenda wapi.

Alipelekwa kwenye duka moja ambapo alikuta kuna suti nzuri imeandaliwa na akaambiwa avae. Baada ya kuvaa, Edger alimchukua Edwin mpaka mwenye ofisi moja ambayo ilikuwa imepambwa vizuri mno kana kwamba kuna jambo linaendelea pale. Walipoingia ndani walimkuta baba mmoja wa makamo kidogo anawasubiri. Baada ya kuingia Edger alindoka na akamwambia Edwin asubiri pale. Edger alirudu muda wa saa 9:15 mchana akiwa na Editrin.

Editrin na Edwin hawakuamini kuwa wamekutana tena. Walikumbatiana huku wakilia, wakiwa hawajui kinachondelea, yule baba aliyekuwepo pale ofisini alisema waache kupoteza muda. Waligeuka na kumtazama.

Walishangaa vyeti vya ndoa vikiletwa na wakambiwa ni ndoa inatakiwa kufungwa pale. Editrin hakuamini lakini alifurahi na kumshukuru sana kaka yake Edger maana aliona hii ndiyo nafasi pekee ya yeye kukwepa ndoa ya lazima kutoka kwa baba yake.

      Kweli ndoa ilifungwa, na baada ya kufunga ile ndoa ya kiserikali, Edger aliandaa hotel nzuri sana kwaajili ya shemeji yake Edwin na dada yake na akalipia kwa muda wa wiki moja. Aliwaambia wasijali kuhusu baba yeye atajua cha kufanya.

Siku iliyofuata Edger alikwenda kwa baba yake na kumwambia kuwa Editrin amekwisha olewa. Mr. Edward alichanganyikiwa na akaamuru mwanaye Edger apelekwe polisi.

Editrin hakujua kinachoendelea nyumbani kwao na hakutaka hata kuwasha simu yake maana Kaka yake alimwambia azime simu kwanza mpaka hasira ya baba ipungue. Baada ya miezi miwili kupita aliamua kwenda nyumbani kwao kuwasalimia maana wakati huo alikuwa anaishi na Edwin Dodoma mjini.

Alipofika nyumbani hakumkuta baba yake. Hivyo, alipata muda mrefu sana wa kuongea na mama yake, ambaye alimueleza mambo yote yaliyotokea, na kwa wakati huo Edger alikuwa kasha tolewa polisi ila alikuwa Iringa kwenye mambo ya kazi. Eliana alimwambia editrin kuwa Edger alikuwa anatarajia kuoa siku chache tu zijazo japo yeye alikuwa anaoa mtoto wakitajiri aliyeitwa Edina. Editrin alifurahi sana kusikia kaka yake anaoa.

 Wakiwa wanaendelea kuzungumza Mr. Edward aliingia, lakini hakuonesha kushtuka wala kukasirika, bali aliwasalimia tu na kupita. Editrin aliogopa kidogo hivyo aliaga na kuondoka kurudi Dodoma.

Siku ya harusi ya kaka yake aliamua kwenda na mume wake Edwin kwenye harusi. Harusi ilikuwa nzuri na yakifahari sana. Usiku walikwenda ukumbini, wakiwa ukumbini Mr. Edward alikwenda kwa binti yake, na kwa mara ya kwanza aliuliza "huyu ndiyo mkwe wangu?" Editrin alijibu "ndiyo" akiwa na hofu sana. Mr. Edward alitabasamu na kusema "karibu sana kijana wangu nimefurahi kukuona" Kisha akatoa mkono wa karibu kwa Edwin.

Edwin na Editrin walishangaa sana. Edwin kimoyo moyo alimshukuru Mungu sana. Baada ya harusi kupita walirudi nyumbani kwao Dodoma.

 Baada ya mwaka kupita Editrin alipata mtoto wakiume ambaye alipewa jina la Elvine, Edwin ndiye aliyetoa jina hilo, na alisema kuwa mwanaye anataka amlee vizuri ili aje kuwa mtumishi mzuri sana wa Mungu.

Baada ya Editrin kujifungua mtoto huyo, wazazi wa Edwin ndiyo waliokuwa wa kwanza kuja na kumuuguza Editrin na walimuonesha upendo sana. Baada ya wiki kupita ndipo wazazi wa Editrin pia walikuja kumsalimia binti yao huku wakiwa na zawadi nyingi sana.

Baada ya miezi mitatu kupita Edwin aliweza kuajiriwa na serikali kama mwana sheria wa serikali, lakini hakutaka mkewe afanye kazi. Hivyo, walifungua duka kubwa la jumla maeneo ya nanenane-Dodoma 

Edwin alifanya kazi mwezi mmoja tu, na ndipo Editrin alipopata taarifa kuwa mumewe amepotea katika mazingira ya kutatanisha. Wakiwa wanaendelea kumtafuta walipata taarifa kuwa kuna mtu amekutwa kachomwa moto jijini Dar es salaam karibu na bahari na alikuwa amevaa saa ya Edwin maana sura haikutazamika kwa namna alivyoungua. Taarifa ile ilithibitisha kuwa aliyekuwa kafariki ni Edwin tena kwa kuuwawa kikatili.

Editrin alilia sana, hivyo waliuchukua mwili ule na kuuzika.

     Editrin baada ya kumpoteza mume wake aliamua kurudi nyumbani kwao. Alipokelewa vizuri tu. Lakini baada ya wiki moja kupita Mr. Edward alisema hahitaji kuona mtoto wa masikini kwenye nyumba yake hivyo mtoto apelekwe kwenye kituo cha wototo yatima na yeye aolewe na mtu mwingine ambaye yeye kama baba kamuandaa.

Editrin hakuwa tayari. Hivyo siku ya jumapili alikwenda kanisani na kutoa nadhiri kwa Mungu kuwa Elvine akikua vyema basi atakuwa ni Mtumishi wa Mungu, na yupo tayari kwa lolote ila mwanaye hato ruhusu apelekwe kituo cha watoto yatima. Ni bora hata alelewe na mtu mwingine ila sio kituo cha watoto yatima kwakuwa mwanaye siyo yatima. Na katika ndoto zake alitamani mtoto huyu awe na hatima njema na awe msaada kwa wengine. Alimuweka mtoto katika nadhiri ya kuwa mtumishi katika huduma ya uchungaji kwakuwa alitamani Elvine aje atimize ndoto za baba yake (Edwin).

Baada ya kurudi nyumbani aligundua kuwa kifo cha mumewe, Edwin, baba yake ni muhusika na ndiye alipanga mipango yote. Aligundua hili baada ya kusikia ugomvi kati ya baba yake na mama yake, wakati mama yake akiwa anamlaumu Mr. Edward kwa kuharibu maisha ya binti aliyemzaa mwenyewe lakini Edward alisema tu! hayo yameshapita na yeye hajui chochote ila anachotaka ni binti yake aolewe kiheshima. Jambo hili lilithibitisha kuwa mama yake alikuwa wakwanza kujua jambo hili, japo aliogopa kumwambia binti yake. Editrin aliumia sana na ndipo alipoamua kutoroka kwao na kwenda kuishi Iringa. Jambo lile lilimfanya asimwamini mtu yeyote kutoka kwao. Pia alikumbuka kuwa miaka kadhaa iliyopita baada ya yeye kuja iringa kaka yake alifanikiwa kufahamu mahali alipo na alishawishiwa sana na Edger kurudi nyumbani lakini hakuwa tayari kufanya hivyo. Hivyo alimwambia Edger kuwa asije tena kwake maana hataki mwanaye ateseke tena na wala hataki kukumbuka yaliopita, kwahiyo toka siku hiyo hakuonana tena na Edger wala mtu yeyote wa kwao, maana Edger alichukia sana baada ya kuona msimamo wa mdogo wake kuamua kujitenga hivyo aliondoka na hakuja tena. Lakini pasipo Editrin kujua, Edger ndiye aliyepigwa jiwe la kichwa na Elvine ule usiku wakati Elvine alipokuwa anatoka kwa rafiki yake Efraim.

*    *    *    *    *    *    *   *

     Elvine alishituka na akajikuta hospitali. Alishangaa kuona kazungukwa na watu asiowajua kabisa, na cha ajabu zaidi walikuwa ni wachina wanne na mwafrika mmoja. Aliogopa sana kisha akauliza "hapa ni wapi?". Watu wale walionesha tabasamu lililoashiria furaha ya yeye kuamka, lakini walionesha dhahiri kuwa hawakuwa wanamuelewa kabisa anachoongea....

Sehemu ya  nne >>>>>Itaendelea jumatatu. Usikose kufatilia.

Kupata mwendelezo wake bofya hapa



 Hadithi hii imetungwa na kuandikwa na JACQUELINE JOHN.

Mwimbaji na mtunzi wa nyimbo, mashairi, Hadithi (simulizi) na ngonjera.

 Mawasiliano:

Whatsapno. >>>>> +255789523850. Normal >>>>>+255747313148.

 Na imehaririwa na MIGONGO ELIAS. Mhariri.

Mawasiliano:

Whatsapno. >>>>> +255767653697. Normal >>>>>+255783327456.

    GeT tO tHe NeXt LeVeL!

 

Kama umejifunza kitu shiriki nasi katika comment hapo chini. Ili tupate kujifunza kwa pamoja na kuboresha zaidi.

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

      

 

    

 

 

 

    

   

    

   

 

 

Popular posts from this blog

GHARAMA 5 ZA KUUFIKIA UKUU UNAOUTAKA.

USIKUBALI KUAJIRIWA KABLA HUJASOMA HAPA.

SIRI ILIYOPO NYUMA YA TABASAMU.